79 SUURATUN NAAZIA'AT

Sura hii imeteremshwa Makka, na ina Aya 46

Kwa jina la Mwenyeezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

1. Naapa kwa wale (Malaika) wavutao kwa nguvu.

2. Na kwa wale wanaotoa kwa upole.

3. Na kwa wale wanao ogelea sana.

4. Na kwa wale wenye kutangulia zaidi.

5. Na kwa wale wenye kupanga mambo.

6. Siku kitakapotetemeka cha kutetemeka.

7. Kifuate cha kufuatia.

8. Siku hiyo nyoyo zitapigapiga (kwa khofu).

9. Macho yake yatainama chini.

10. (Makafiri) wanasema Je, kweli tutarudishwa hali yetu ya kwanza?

11. Hata tukiwa mifupa mibovu?

12. Wanasema: Basi marudio hayo ni yenye khasara.

13. Hakika huo utakuwa ni ukelele mmoja tu.

14. Mara watakuwa juu ya ardhi.

15. Je, imekufikia hadithi ya Musa?

16. Mola wake alipomwita katika bonde takatifu la Tuwaa.

17. (Akamwambia) Nenda kwa Firaun, hakika yeye amezidi kuasi.

18. Kisha mwambie: Je. unapenda kujitakasa?

19. Nami nitakuongoza kwa Mola wako ili umche.

20. Rasi alimuonyesha Miujiza mikubwa.

21. Lakini alikadhibisha na akaasi.

22. Kisha alirudi nyuma akaenda.

23. Ndipo aliwakusanya akatangaza.

24. Akasema: Mimi ndiye Mola wenu mkubwa.

25. Mara Mwenyeezi Mungu akamuadhibu kwa adhabu ya Akhera na ya dunia.

26. Kwa hakika katika hayo mna mazingatio kwa yule anayeogopa.

27. Je, nyinyi ni wenye umbo gumu zaidi, au mbingu alizozijenga?

28. Akainua kimo chake na akaitengeneza vizuri.

29. Na akautia giza usiku wake, na akautokeza mchana.

30. Na ardhi baada ya hayo akaitandaza.

31. Akatoa ndani yake maji yake na malisho yake.

32, Na milima akaiimarisha.

33. Kwa manufaa yenu na wanyama wenu.

34. Lakini utakapofika ule msiba mkubwa.

35. Siku ambayo mtu atakumbuka aliyotenda.

36. Na Moto mkali utaonyeshwa kwa yule anayeuona.

37. Ama yule aliyeasi.

38. Na akapenda zaidi maisha ya dunia.

39. Basi kwa hakika Jahannam ndiyo makao.

40. Na ama yule aliyeogopa kusimama mbele ya Mola wake, na akaikataza nafsi matamanio (maovu).

41. Basi kwa hakika Pepo ndiyo makazi (yake).

42. Wanakuuliza juu ya Kiyama kutokea kwake kutakuwa lini.

43. Una haja gani kukitaja.

44. Mwisho wake ni kwa Mola wako.

45. Wewe ni Muonyaji tu kwa yule anayeiogopa.

46. Siku watakapoiona watakuwa kama kwamba hawakukaa ila jioni moja au mchana wake!