20. SUURA TWAHA

Sura hii imeteremstiwa Makka, na ina Aya 135.

Kwa jina la Mwenyeezi Mungu, Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu.

1. Twaaha

2. Hatukukuteremshia Qur'an ili upate mashaka.

3. Bali iwe mawaidha kwa mwenye kunyenyekea.

4. Mteremsho utokao kwa yule aliyeumba ardhi na mbingu zilizoinuka.

5. Mwenyeezi Mungu Mwingi wa rehema aliyekamilisha (uumbaji wake) katika Arshi.

6. Ni vyake vilivyomo mbinguni na vilivyomo ardhini na vilivyomo kati yake na vilivyomo chini ya ardhi.

7. Na ukinena kwa sauti kubwa basi hakika yeye anajua yaliyo siri na yaliyofichikana zaidi.

8. Mwenyeezi Mungu hakuna aabudiwaye isipokuwa yeye tu, anayo majina mazuri.

9. Na je, imekufikia hadithi ya Musa?

10. Alipouona moto na akawaambia watu wake: Ngojeni, hakika nimeona moto, huenda nitakuleteeni kijinga katika huo au nitapata muongozo kwenye moto.

11. Basi alipoufikia akaitwa: Ewe Musa!

12. Bila shaka Mimi ndiye Mola wako basi vua viatu vyako, hakika wewe upo katika bonde Tuwaa lililotakasika.

13. Nami nimekuchagua, basi yasikilize unayoletewa Wahyi.

14. Kwa hakika mimi ndiye Mwenyeezi Mungu hakuna aabudiwaye ila Mimi tu, basi niabudu na simamisha swala kwa kunitaja.

15. Bila shaka Kiyama kitakuja, nataka kusudi kukificha ili kila nafsi ilipwe kwa yale iliyoyafanya.

16. Basi asikuzuie katika hayo yule asiye yaamini na afuataye matamanio yake, usije ukaangamia.

17, Na ni nini kilichomo mkononi mwako wa kulia ewe Musa?

18. Akasema: Hii ni fimbo yangu ninaegemea na ninaangushia majani kwa ajili ya wanyama wangu, tena ninaitumia kwa matumizi mengine.

19. Akasema: Itupe ewe Musa.

20. Akaitupa, mara ikawa nyoka anayekimbia.

21. Akasema: Ikamate wala usiogope, tutairudisha hali yake ya kwanza.

22. Na bandika mkono wako kwenye kwapa lako utatoka mweupe pasipo ubaya Muujiza mwingine.

23. Ili tukuonyeshe Miujiza yetu mikubwa mikubwa.

24. Nenda kwa Firaun bila shaka yeye amepindukia mipaka.

25. Akasema: Ee Mola wangu! nipanulie kifua changu.

26. Na unifanyie wepesi kazi yangu.

27. Na ufungue fundo katika ulimi wangu.

28. Wapate kufahamu kauli yangu.

29. Na uniwekee waziri katikajamaa zangu.

30. Ndugu yangu Harun.

31. Nitie nguvu kwa (ndugu yangu).

32. Na umshirikishe katika kazi yangu.

33. Ili tukutukuze sana.

34. Na tukutaje kwa wingi.

35. Hakika wewe unatuona.

36. Akasema: Hakika umepewa maombi yako, ewe Musa.

37. Na hakika tulikufanyia hisani mara nyingine.

38. Tulipomfunulia mama yako yanayo funuliwa.

39. Kwamba Mtie (mwanao) sandukuni, kisha litie mtoni, na mto utamtupa ufukweni ili amchukue adui yangu na adui yake. Na nimekutilia mapenzi kutoka kwangu, na ili ulelewe machoni mwangu.

40. (Kumbuka) dada yako alipo kwenda na akasema: Je, nikujulisheni atakayemlea? Na tukakurudisha kwa mama yako ili macho yake yaburudike wala asihuzunike. Na ulimuua mtu na tukakuokoa katika huzuni na ukakujaribu kwa majaribio (mengi). Na ukakaa miaka mingi kati ya watu wa Madyan, kisha umefikia kama ilivyokadiriwa ewe Musa.

41. Na nimekuchagua kwa ajili yangu.

42. Nenda wewe na ndugu yako pamoja na hoja zangu wala msichoke kunikumbuka.

43. Nendeni kwa Firaun, bila shaka amepindukia mipaka.

44. Na kamwambieni maneno laini huenda atashika mawaidha au ataogopa.

45. Wakasema: Ewe Mola wetu! hakika sisi tunaogopa asije kutufanyia matata tu kutudhulumu.

46. Akasema: Msiogope bila shaka Mimi ni pamoja nanyi, nasikia na naona.

47. Basi mwendeeni na mwambieni: Kwa hakika sisi ni Mitume wa Mola wako, kwa hiyo wapeleke pamoja nasi wana wa Israeli na usiwaadhibu. Hakika tumekuletea Muujiza utokao kwa Mola wako, na amani iwe juu ya anayefuata muongozo.

48. Hakika tumeletewa Wahyi kwamba: Adhabu itampata yule anayekataa na kupuuza.

49. (Firaun) akasema; Mola wenu ni nani ewe Musa?

50. Akasema: Mola wetu ni yule aliyekipa kila kitu umbo lake kisha akaongoza.

51. Akasema: Basi ni hali gani ya vizazi vya kwanza.

52. Akasema: Elimu yake iko kwa Mola wangu katika Kitabu, Mola wangu hapotei wala hasahau.

53. Ambaye amekufanyieni ardhi kuwa tandiko na amekuwekeeni humo njia, na akayateremsha maji kutoka mawinguni. Na kwa hayo tukaotesha namna za mimea mbali mbali.

54. Kuleni na walisheni wanyama wenu, bila shaka katika hayo mna dalili kwa wenye akili.

55. Katika (ardhi) hiyo tumekuumbeni, na humo tutakurudisheni na kutoka humo tutakutoeni mara nyingine.

56. Na hakika tulimuonyesha (Firaun) Miujiza yetu yote lakini alikadhibisha na akakataa.

57. Akasema: Umetujia kututoa katika nchi yetu kwa uchawi wako ewe Musa?

58. Basi sisi tutakuletea uchawi kama huo, kwa hiyo ufanye ahadi ya mkutano baina yetu na yako ambayo tusiivunje sisi wala wewe (katika) mahala patakapokuwa sawa.

59 (Musa) akasema: Miadi yenu ni siku ya mapambo na watu wakusanywe asubuhi.

60. Basi Firaun akarudi na akakusanya hila yake kisha akaja.

61. Musa akawaambia: Ole wenu! msizushe uongo juu ya Mwenyeezi Mungu, asije akakufuteni kwa adhabu, na amekwisha shindwa anayezua uongo.

62. Basi (wale wachawi) wakazozana kwa shauri lao wenyewe kwa wenyewe na wakanong'onezana kwa siri.

63. Wakasema: Hakika hawa wawili ni wachawi, wanataka kukutoeni katika nchi yenu kwa uchawi wao, na kuondoa desturi yenu iliyo bora kabisa.[1]

64. Kwa hiyo kusanyeni hila zenu, kisha mfike kwa kujipanga safu na kwa hakika amefuzu leo atakayeshinda.

65. Wakasema: Ewe Musa! je, utatupa au tutakuwa sisi wa kwanza kutupa?

66. (Musa) akasema: Bali tupeni! Mara kamba zao na fimbo zao zikaonekana mbele yake, kwa uchawi wao zikienda rnbio.

67. Basi Musa akaona khofu katika nafsi yake.

68. Tukasema: Usiogope, hakika wewe ndiye mwenye kushinda.

69. Na kitupe kilicho katika mkono wako wa kulia kitavimeza walivyovitengeneza, hakika wametengeneza hila za mchawi, wala mchawi hatafaulu popote afikapo.

70. Basi wachawi wakaangushwa kusujudu, wakasema: Tumemwamini Mola wa Harun na Musa.

71. (F'iraun) Akasema: Jee, mnamwamini kabla sijakupeni ruhusa! Bila shaka yeye ndiye mkubwa wenu aliyekufunzeni uchawi. Kwa hiyo, hakika nitakukateni mikono yenu na miguu yenu kwa kutofatisha na lazima nitakusulubuni katika mashina ya mitende, na bila shaka mtajua ni nani katika sisi aliye mkali wa kuadhibu na kuiendeleza.

72. Wakasema: Hatukutangulizi kabisa juu ya hoja wazi wazi zilizotufikia na kuliko yule aliyetuumba, basi fanya unavyotaka kufanya, unaweza kutoa hukumu inayohusiana na maisha haya ya dunia tu.

73. Kwa hakika tumemwamini Mola wetu ili atusamehe makosa yetu na uchawi uliotulazimisha kuufanya, na Mwenyeezi Mungu ndiye bora na wa kudumu.

74. Hakika atakayekuja kwa Mola wake hali ya kuwa ni muovu, basi kwa hakika (malipo) yake (huyo) ni Jahannam, hatakufa wala hataishi maisha mazuri.

75. Na atakayemjia hali ya kuwa muumini aliyefanya vitendo vizuri, basi hao ndio watakaopata vyeo vya juu.

76. Bustani za kudumu zipitazo mito chini yake, wakae humo milele, na hayo ni malipo ya mwenye kujitakasa.

77. Na hakika tulimpelekea Wahyi Musa kwamba wapeleke usiku waja wangu, na ukawafanyie njia kavu baharini, usiogope kukamatwa wala usiogope lolote.

78. Basi Firaun akawafuata pamoja na majeshi yake, na kikawafudikiza katika bahari kilichowafudikiza.

79. Na Firaun akawapoteza watu wake wala hakuwaongoza.

80. Enyi wana wa Israel! hakika tumewaokoeni na adui yenu na tukakuahidini upande wa kulia wa mlima na tukakuteremshieni Manna na Salwa.

81. Kuleni katika vitu vizuri tulivyokuruzukuni wala msiiruke mipaka katika hayo isije ikakushukieni ghadhabu yangu. Na inayemshukia ghadhabu yangu, basi ameangamia.

82. Na hakika mimi ni mwenye kusamehe sana kwa anayetubia na kuamini na kutenda mema, tena akashika muongozo.

83. Na nini kilichokuharakisha kwa kuwaacha watu wako ewe Musa?

84. Akasema: Hao wapo nyuma yangu wananifuata, na nimeharakia kwako, Mola wangu, ili uwe radhi.

85. Akasema: (Mwenyeezi Mungu) Bila shaka tumewajaribu watu wako baada yako, na Msamaria amewapoteza.

86. Basi Musa akarudi kwa watu wake kwa ghadhabu (na) kusikitika. Akasema: Enyi watu wangu! Je, Mola wenu hakukuahidini ahadi nzuri? Je, imekuwa ndefu kwenu ahadi hiyo au mmetaka iwashukie ghadhabu kutoka kwa Mola wenu, kwa hiyo mmevunja ahadi yangu?

87. Wakasema: Sisi hatukuvunja ahadi yako kwa hiari yetu, lakini tulibebeshwa mizigo ya mapambo ya watu, tukaitupa na hivyo ndivyo alivyotia Samir.

88. Na akawatolea ndama kiwili wili chenye sauti, na wakasema: Huyu ndiye mungu wenu na mungu wa Musa, lakini alisahau.

89. Je, hawakuona yakuwa (ndama huyo) hakuwarudishia neno wala hakuweza kuwadhuru wala kuwafaa?

90. Na bila shaka Harun alikwisha waambia zamani: Enyi watu wangu! hakika nyinyi mmefitinishwa tu kwa kitu hiki na kwa hakika Mola wenu ni Mwingi wa rehema basi nifuateni na tiini amri yangu.

91. Wakasema: Hatutaacha kabisa kukiabudu mpaka Musa arejee kwetu.

92. (Musa aliporejea) akasema: Ewe Harun! ni nini kilichokuzuia ulipowaona wakipotea.

93. Usinifuate? Je, umeasi amri yangu?

94. Akasema: Ewe mwana wa mama yangu usinishike ndevu zangu, wala kichwa changu, kwa hakika mimi niliogopa usije kusema: Umewafarikisha wana wa Israel na hukungojea kauli yangu.

95. (Musa) akasema: Ewe Msamaria, basi nia yako ilikuwa nini?

96. Akasema: Niliona wasiyoyaona na nikashika sehemu chache ya mwendo wa Mtume, kisha nikautupa, na hivyo ndivyo ilinielekeza nafsi yangu.

97. (Musa) akasema: Basi ondoka na kwa hakika utakuwa katika maisha ukisema: Usiniguse, na bila shaka ni ahadi kwako isiyovunjwa. Na mtazame mungu wako uliyeendelea kumuabudu, lazima tutamuunguza kisha tutamzamisha baharini apotee kabisa.

98. Hakika muabudiwa wenu ni Mwenyeezi Mungu tu, ambaye hakuna aabudiwaye ila yeye tu, anakijua kila kitu kwa elimu. (yake).

99. Kama hivyo tunakuhadithia katika khabari za (mambo) yaliyotangulia na bila shaka tumekupa mawaidha kutoka kwetu.

100. Atakayejitenga nayo, basi kwa hakika atabeba mzigo siku ya Kiyama.

101. Watakaa humo milele, na ni vibaya kwao siku ya Kiyama kubeba mzigo.

102. Siku itakapopigwa baragumu na tutawakusanya waovu siku hiyo, hali macho yao ya kibuluu.

103. Watanong'onezana wao kwa wao: Hamkukaa ila (siku) kumi tu.

104. Sisi tunajua sana watakayosema, atakaposema mbora wao katika mwendo: Nyinyi hamkukaa ila siku moja tu.

105. Na wanakuuliza khabari za milima basi waambie: Mola wangu ataivunja vunja.

106. Na ataiacha (ardhi) uwanda uliokaa sawa sawa.

107. Hutaona humo kombo wala miinuko.

108. Siku hiyo watamfuata mwitaji asiye na upotovu, na zitanyenyekea sauti kwa Mwenyeezi Mungu na hutasikia ila mnong'ono.

109. Siku hiyo hautafaa uombezi ila kwa yule anayemruhusu Mwenyeezi Mungu tu na kuiridhia kauli yake.

110. Anajua yaliyo mbele yao na yaliyo nyuma yao, wala hawawezi kumjua (Mwenyeezi Mungu) vilivyo.

111. Na nyuso zitadhalilika mbele ya (Mwenyeezi Mungu) aliye hai, wa milele, na ameshindwa aliyefanya dhuluma.

112. Na atakayefanya vitendo vizuri, naye ni muumini, basi hataogopa dhulma wala kunyimwa (haki yake).

113. Na (mfano) kama huo tuliiteremsha Qur'an kwa uwazi, na tumeeleza humo (mara kwa mara) maonyo ili wapate kuogopa au ili iwatolee ukumbusho.

1 14. Basi atukuzwaye ni Mwenyeezi Mungu, Mfalme wa haki wala usifanye haraka kwa Qur'an kabla haujamalizika kukufikia Wahyi wake, na (uombe) useme: Mola wangu! nizidishie elimu.

15. Na bila shaka tulimuahidi Adamu zamani basi akasahau, lakini  hatukumuona mwenye nia (ya kuvunja ahadi).

116. Na (kumbukeni) tulipowaambia Malaika. Mtiini Adamu, basi wakamtii isipokuwa Iblis alikataa.

117. Basi tukasema: Ewe Adamu! hakika huyu ni adui yako na ya mke wako, hivyo asikutoeni katika bustani mkaingia mashakani.

1 18. Hakika hutakuwa mwenve njaa humo wala hutakuwa uchi.

119. Na kwa hakika hutapata kiu humo wala hutapata joto.

120. Basi shetani akamtia wasi wasi, akamwambia: Ewe Adamu! Je, nikujulishe mti wa milele na ufalme usiokoma?

121. Ndipo wakaula wote wawili na uchi wao ukawadhihirikia na wakaanza kujibandika majani ya bustani, na Adamu akamuasi Mola wake na akapotea.

122. Kisha Mola wake akamchagua na akamkubalia toba na akamuongoza.

123. Akasema: Ondokeni humo nyote nyinyi kwa nymyi ni maadui, na kama ukikufikieni muongozo kutoka kwangu, basi atakayeufuata muongozowangu hatapotea wala hatapata taabu.

124. Na atakayejiepusha na mawaidha yangu, basi kwa hakika atapata maisha yenye dhiki, na siku ya Kiyama tutamfufua hali ya kuwa kipofu.

125. Aseme: Ee Mola wangu! mbona umenifufua kipofu na hali nilikuwa nikiona?

126. (Mwenyeezi Mungu) atasema; Hivyo ndivyo, zilikufikia Aya zetu lakini ukazisahau, na kama hivyo leo unasahauliwa.

127. Na hivyo ndivyo tutakavyomlipa apitae kiasi na asiyeamini Aya za Mola wake, na bila shaka adhabu ya Akhera ni kali zaidi na iendeleayo sana.

128. Je, haikuwabainikia ni vizazi vingapi tulivyoviangamiza kabla yao, waliokuwa wakitembea katika maskani zao? Bila shaka katika hayo mna dalili kwa wenye akili.

129. Na kama si neno lililotangulia kutoka kwa Mola wako na muda uliowekwa, lazima ingefika adhabu.

130. Basi yavumilie hayo wayasemayo, na utukuze kwa sifa za Mola wako kabla halijatoka jua na kabla halijatua, na nyakati za usiku pia umtukuze, na katikati ya mchana ili uridhike.

131. Wala usivikodolee macho yako tulivyowastareheshea watu wengi miongoni mwao, ni mapambo ya maisha ya dunia, ili tuwajaribu kwa hayo, na riziki ya Mola wako ni bora mno na iendeleayo.

132. Na waamrishe watu wako kuswali, na uendelee kwa hayo, hatukuombi riziki bali sisi tunakuruzuku, na mwisho mwema ni kwa mcha Mungu.

133. Na (makafiri) wakasema: Kwa nini hakutuletea Muujiza kutoka kwa Mola wake? Je, haikuwafikia dalili wazi ya yale yaliyokuwa katika Vitabu vya kale?

134. Na lau kama tungeliwaangamiza kwa adhabu kabla yake (Mtume) wangesema: Ee Mola wetu mbona hukutuletea Mtume tukazifuata Aya zako kabla sisi kudhalilika na kufedheheka.

135. Sema: Kila mmoja anangoja, basi ngojeni (nanyi pia) na mtajua ni nani mwenye njia iliyo sawa na ni nani aliyeongoka.


[1] Aya 63.

 MWANA AISHA INAMTATIZA QUR'AN

Amesema mwana Aisha: kusoma, "INNA HADHAANI LASAHIRANI" ni makosa ya uandishi. Akasema Uthmani bin Affan: Katika msahafu kuna makosa, watarekebisha waarabu kwa lugha yao.

Taz: Tafsirul Qurtubi       J.ll Uk. 216

KWA SOMO LA LUGHA!

INNA: ina kazi mbili,

a) Ni harfu tawkiid, inanasibisha jina na kurufaisha khabar.

b) Ni harfu ya jawabu, kwa maana ya "NAAM" Yaani, ndiyo. Na 'LAM" ilyoko katika "LASAHIRANI" ni harfu zaaid, imezidi.

Taz: Mughunil labiib       J.l Uk. 37-38.

Kwa hiyo, "INNA" iliyoko katika Aya 63 ya Sura Twaaha, ni harfu ya jawabu, na "LAM" katika ''LASAH'IRANl" ni harfu zaidi.