SUURA HUUD

Sura hii imeteremshwa Makka, na ina Aya 123

Kwa jina la Mwenyeezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

1. Alif Lam Ra. Hiki ni Kitabu ambacho Aya zake zimewekwa wazi, kisha zimepambanuliwa kutoka kwa Mwenye hekima, Mwenye ujuzi.

2. Kwamba msiabudu isipokuwa Mwenyeezi Mungu tu. Hakika mimi kwenu ni muonyaji na mtoaji wa khabari njema ninayetoka kwake.

3. Na kwamba muombe msamaha kwa Mola wenu kisha mtubie kwake, atakustarehesheni kwa starehe nzuri mpaka muda maalum, na atampa kila mwenye fadhila fadhili yake. Na ikiwa mtakataa basi nakukhofieni adhabu ya siku kubwa.

4. Marejeo yenu ni kwa Mwenyeezi Mungu, naye ni Mwenye uwezo juu ya kila kitu.

5. Sikilizeni! Hakika wao wanakunja vifua vyao ili wamfiche (Mwenyeezi Mungu). Sikilizeni! wanapojigubika nguo zao anajua wanayoyaficha na wanayoyadhihirisha, hakika yeye ni Mjuzi wa yaliyomo vifuani.

6. Na hakuna mnyama yeyote katika ardhi isipokuwa riziki yake iko juu ya Mwenyeezi Mungu, na anajua makao yake na mapitio yake, yote yamo katika Kitabu dhahiri.

7. Na yeye ndiye aliyeziumba mbingu na ardhi katika nyakati sita, na Arshi yake iko juu ya maji, ili akujaribuni ni nani miongoni mwenu mwenye vitendo bora. Na kama ukisema: Hakika nyinyi mtafufuliwa baada ya kufa, bila shaka waliokufuru watasema: Hayakuwa haya ila ni uchawi uliyo wazi.

 8. Na kama tukiwakawizia adhabu mpaka muda uliohesabiwa, bila shaka watasema: Ni nini kinachoizuia? Sikilizeni siku itakapowafikia haitaondolewa kwao, na yatawazunguka yale waliyokuwa wakiyafanyia rnzaha.

9. Na kama tukimuonjesha mwanadamu rehema kutoka kwetu, kisha tukaiondoa kwake, bila shaka yeye anakuwa mwenye kukata tamaa asiyekuwa na shukrani.

10. Na kama tukimuonjesha neema baada ya madhara yaliyompata, bila shaka husema: Taabu zimeondoka kwangu, kwa hakika yeye ndiye Mwenye kufurahi sana, mwenye kujivuna sana.

11. Isipokuwa wale wanaosubiri na kufanya vitendo vizuri, hao ndio watakaopata msamaha na ujira mkubwa.

 12. Basi huenda utaacha baadhi ya yale yaliyofunuliwa kwako, na kifua chako kitaona dhiki kwa hayo, kwa sababu wanasema: Mbona hakuteremshiwa khazina au kuja Malaika pamoja naye? Hakika wewe ni muonyaji tu, na Mwenyeezi Mungu ndiye Mlinzi wa kila kitu.

13. Je, wanasema: Amekitunga? Sema: Basi leteni sura kumi zilizotungwa mfano wa hii, na waiteni muwezao badala ya Mwenyeezi Mungu ikiwa mnasema kweli.

14. Na kama hawakukuitikieni, basi jueni kwamba kimeteremshwa kwa elimu ya Mwenyeezi Mungu na kwamba hakuna aabudiwaye ila yeye tu, basi je, mtakuwa wanyenyekevu?

15. Wanaotaka maisha ya dunia na mapambo yake, tutawapa (ujira wa) vitendo vyao kamili, na humo wao hawatapunjwa.

16. Hao ndio ambao hawatakuwa na kitu katika Akhera ila Moto, na yataharibika waliyokuwa wakiyatenda. Na yatapotea bure yale waliyokuwa wakiyafanya.

 17. Basi je, mtu aliye na dalili wazi itokayo kwa Mola wake, na anaifuata (dalili) na Shahidi atokaye kwake, na kabla yake kulikuwa Kitabu cha Musa kilichokuwa kiongozi na rehema (atakuwa muongo?). Hao wanamwamini yeye, na atakayemkataa katika makundi ya maadui basi Moto ndio mahala pa miadi yake. basi usiwe na shaka juu ya huyo, hakika hii ni haki itokayo kwa Mola wako, lakini watu wengi hawaamini.

18. Na ni nani dhalimu mkubwa kuliko yule amzuliaya Mwenyeezi Mungu uongo, hao watahudhurishwa mbele ya Mola wao, na mashahidi watasema: Hawa ndio waliomzulia Mola wao uongo. Sikilizeni! laana ya Mwenyeezi Mungu iko juu ya madhalimu.

19. Ambao wanazuilia (watu) njia ya Mwenyeezi Mungu na wanataka ipotoke, na wanaikataa Akhera.

20. Hao hawawezi kuponyoka katika nchi, wala hawana walinzi badala ya Mwenyeezi Mungu, watazidishiwa adhabu. Hawakuwa wakiweza kusikia wala hawakuwa wakiona.

21. Hao ndio waliozitia khasara nafsi zao, na yatawapotea waliyokuwa wakiyazua.

22. Bila shaka hao ndio wenye khasara zaidi katika Akhera.

23. Hakika wale walioamini na kufanya vitendo vizuri na kunyenyekea kwa Mola wao, hao ndio watu wa Peponi, wao watakaa humo milele.

24. Hali ya makundi mawili (haya ya Waislaamu na makafiri) ni kama kipofu na kiziwi na aonaye na asikiae je, hawa wawili wanaweza kuwa sawa katika hili? basi je, hamfikiri?

25. Na bila shaka sisi tulimpeleka Nuhu kwa watu wake, (akawaambia) Hakika mimi kwenu ni muonyaji anayebainisha.

26. Kwamba Msimwabudu isipokuwa Mwenyeezi Mungu tu, hakika mimi ninakukhofieni adhabu ya siku inayoumiza.

27. Hapo wakasema wakubwa wa wale waliokufuru katika kaumu yake: Hatukuoni ila ni rntu tu sawa na sisi, wala hatukuoni ila wamekufuata wale wanaoonekana dhahiri kuwa dhaifu wetu wala hatukuoneni kuwa mnayo ziada juu yetu, basi tunakuoneni kuwa ni waongo.

28. Akasema: Enyi watu wangu! Mnaonaje ikiwa ninayo dalili iliyo wazi itokayo kwa Mola wangu, na amenipa rehema kutoka kwake nayo ikafichika kwenu. Je, tutakulazimisheni (kuikubali) na hali nyinyi mnaichukia?

29. Na enyi watu wangu! sikuombeni mali juu ya (jambo) hili, sina ujira wangu ila kwa Mwenyeezi Mungu, na mimi sitawafukuza wale walioamini, maana wao ndio watakaokutana na Mola wao, lakini mirni ninakuoneni ni watu mnaofanya ujinga.

30. Na enyi watu wangu! ni nani atakayenisaidia mbele ya Mwenyeezi Mungu ikiwa nitawafukuza? je, hamfikiri?

31. Wala sikuambieni kuwa nina khazina za Mwenyeezi Mungu, wala kuwa najua mambo ya ghaibu wala sisemi mimi ni Malaika wala siwasemi wale ambao yanawadharau macho yenu, Mwenyeezi Mungu hatawapa kheri. Mwenyeezi Mungu anajua sana yaliyomo katika nafsi zao, (nikisema hivi) hapo lazima nitakuwa miongoni mwa madhalimu.

32. Wakasema: Ewe Nuhu! Hakika umejadiliana nasi na umezidisha majadiliano nasi, basi tuletee unayotuahidi ukiwa miongoni mwa wakweli.

33. Akasema: Hakika Mwenyeezi Mungu atakuleteeni akipenda, na nyinyi hamtaweza kushinda.

34. Wala haitakufaeni nasaha yangu nikitaka kukunasihini, kama Mwenyeezi Mungu anataka kukuangamizeni. Yeye ndiye Mola wenu, na kwake mtarejeshwa.

35. Je, wanasema ameitunga? Sema: Kama nimeitunga, basi kosa langu ni juu yangu, na mimi ni mbali na makosa mnayoyafanya.

36. Na akaletewa Wahyi Nuhu kuwa hataamini katika watu wako isipokuwa yule aliyekwisha amini, kwa hiyo usisikitike kwa yale waliyokuwa wakiyatenda.

37. Na unda jahazi mbele ya macho yetu na iwe sawa na amri yetu, wala usinisemeze katika wale waliodhulumu, kwa hakika wao watazamishwa.

38. Na akawa anaunda jahazi, na kila wakimpita wakuu wa watu wake wakimkejeli, akasema: Ikiwa nyinyi mnatukejeli, hakika nasi tutakuchekeni kama mnavyotucheka.

39. Basi karibuni mtajua ni nani itakayemfikia adhabu ya kumfedhehesha na itamteremkia adhabu yenye kudumu.

40. Hata ilipofika amri yetu na chemchem ya maji ikabubujika, tukamwambia: Pakia humo wawili wawili dume najike kutoka kila aina, na watu wako wa nyumbani isipokuwa yule ambaye imempitia hukumu, na walioamini, na hawakuamini pamoja naye ila wachache tu.

41. Na akasema: Pandeni humo, kwajina la Mwenyeezi Mungu kuwe kwenda kwake na kusimama kwake: Hakika Mola wangu ni Mwingi wa kusamehe, Mwenye kurehemu.

42. Nayo (ikawa) inakwenda nao katika mawimbi kama milima. Na Nuhu akamwita mwanaye aliyekuwa mbali. Ewe mwanangu! panda pamoja nasi wala usiwe pamoja na makafiri.

43. Akasema: Nitaukimbilia mlima utakaonilinda na maji. Akasema leo hakuna wa kulindwa na amri ya Mwenyeezi Mungu isipokuwa yule atakaye mrehemu mara wimbi likaingia kati yao na akawa miongoni mwa waliogharikishwa.

44. Na ikasemwa: Ewe ardhi! meza maji yako, na ewe mbingu! zuia, na maji yakadidimia chini, na amri ikapitishwa, na (jahazi) likasimama juu ya (mlima wa) judi, na ikasemwa: Wapotelee mbali watu waliodhulumu.

45. Na Nuhu akamuomba Mola wake, akasema: Ewe Mola wangu! hakika mwanangu ni katika watu wa nyumbani kwangu, na hakika ahadi yako ni haki, na Wewe ni Mwenye haki kuliko Mahakimu.

46. Akasema: Ewe Nuhu! hakika huyo si miongoni mwa watu wako, hakika yeye ni (mwenye) mwendo usio mzuri, basi usiniombe jambo usilo na ujuzi nalo, mimi nakunasihi usije ukawa miongoni mwa wajinga.

47. (Nuhu) akasema; Ee Mola wangu! hakika mimi najikinga kwako nisije kukuomba nisiyoyajua, na kama hutanisamehe na kunirehemu, nitakuwa miongoni mwa watakaopata khasara.

48. Ikasemwa: Ewe Nuhu! shuka kwa salama itokayo kwetu na baraka nyingi juu yako na juu ya watu walio pamoja nawe. Na zitakuwako umma tutakazo zistarehesha, kisha zitawashika kutoka kwetu adhabu yenye kuumiza.

49. Hizo ni katika khabari za ghaibu tunazo kufunulia. Hukuwa ukizijua, wewe wala watu wako kabla ya hii (Qur'an kuteremshwa). Basi subiri, hakika mwisho (mwema) ni kwa wamchao (Mwenyeezi Mungu).

50. Na kwa A'di (tulimpeleka) ndugu yao Hudi akasema: Enyi watu wangu! mwabuduni Mwenyeezi Mungu, nyinyi hamna Mungu isipokuwa yeye tu. Hamkuwa nyinyi ila ni watungao uongo tu.

51. Enyi watu wangu! sikuombeni ujira juu ya haya haukuwa ujira wangu ila kwa yule aliyeniumba, basi je, hamfahamu?

52. Na enyi watu wangu! ombeni msamaha kwa Mola wenu, kisha mtubie kwake atakuleteeni mawingu yateremshayo mvua tele, na atakuzidishieni nguvu juu ya nguvu zenu, wala msigeuke kuwa waovu.

53. Wakasema: Ewe Hudi! Hujatuletea dalili iliyo wazi, wala sisi hatuwezi kuiacha rniungu yetu kwa usemi wako, wala sisi hatukuamini wewe.

54. Hatusemi ila baadhi ya miungu yetu imekutia balaa. Akasema: Hakika mimi namshuhudisha Mwenyeezi Mungu nanyi shuhudieni kwamba mimi niko mbali na hao mnaowashirikisha.

55. Kinyume chake, basi nyote nifanyieni hila kisha msinipe muhula.

56. Hakika mimi nimemtegemea Mwenyeezi Mungu, Mola wangu na Mola wenu, Hakuna mnyama yeyote isipokuwa yeye anamwendesha atakavyo. Bila shaka Mola wangu yuko juu ya njia iliyonyooka.

57. Na kama watarudi nyuma, basi nimekwisha wafikishieni niliyotumwa nayo kwenu, na Mola wangu atawafanya makhalifa watu wengine wasiokuwa nyinyi, wala nyinyi hamtaweza kumdhuru hata kidogo, hakika Mola wangu ni Mwenye kuhifadhi kila kitu.

58. Na ilipofika amri yetu, tukamuokoa Hudi na wale walioamini pamoja naye kwa rehema itokayo kwetu, na tukawaokoa katika adhabu ngumu.

59. Na hao ndio A'di, walikanusha Aya za Mola wao, na wakawaasi Mitume wake na wakafuata amri ya kila jabari mkaidi.

60. Na wakafuatishiwa laana katika dunia hii na siku ya Kiyama, sikilizeni! hakika Adi walimkufuru Mola wao, sikilizeni! ni maangamio kwa Adi kaumu ya Hudi.

61. Na kwa Thamudi (tukampeleka) ndugu yao, Saleh akasema Enyi watu wangu mwabuduni Mwenyeezi Mungu, nyinyi hamna Mungu ila yeye tu. yeye ndiye aliyekuumbeni katika ardhi, na akakukalisheni humo, basi muombeni msamaha, kisha mrejee kwake. Hakika Mola wangu yu karibu Mwenye kupokea (maombi).

62. Wakasema: Ewe Saleh! bila shaka ulikuwa unayetarajiwa kati yetu kabla ya haya. Je, unatukataza kuabudu waliowaabudu baba zetu? Na hakika sisi tumo katika shaka yenye kuhangaisha kwa hayo unayotuitia.

63. Akasema: Enyi watu wangu! Mnaonaje ikiwa ninayo dalili iliyo wazi itokayo kwa Mola wangu, na amenipa rehema kutoka kwake, basi ni nani atakayenisaidia kwa Mwenyeezi Mungu kama nikimuasi? basi hapo hamtanizidishia ila khasara.

64. Na enyi watu wangu! huyu ngamia wa Mwenyeezi Mungu ni ishara kwenu basi mwacheni ale katika ardhi ya Mwenyeezi Mungu wala msimguse kwa ubaya isije ikakuangamizeni adhabu iliyo karibu.

65. Wakamchinja, basi (Saleh) akasema: Stareheni katika mji wenu kwa siku tatu, hiyo ni ahadi isiyokadhibishwa.

66. Basi ilipofika amri yetu, tukamuokoa Saleh na wale walioamini pamoja naye kwa rehema yetu, na pia tukawaokoa katika fedheha ya siku hiyo. Hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kushinda.

67. Na wale waliodhulumu uliwaangamiza ukelele, na wakawa ndani ya majumba yao wameanguka kifudifudi.

68. Kama kwamba hawakuwamo. Sikilizeni! hakika Thamudi walimkufuru Mola wao, sikilizeni! Thamudi wamepotelea mbali.

69. Na bila shaka wajumbe wetu walimwendea Ibrahim kwa khabari njema, wakasema Salaam akasema (pia juu yenu iwe) Salaam, na hakukaa ila akaleta ndama aliyeokwa.

70. Basi alipoona mikono yao haikifikii chakula aliwatilia shaka, na akawaonea khofu.Wakasema; Usiogope, hakika sisi tumetumwa kwa watu wa Luti.

71. Na mkewe (lbhimu , Sara) alikuwa wima akacheka, basi tukampa khabari njema ya kuzaliwa Isihaqa na baada ya Isihaqa, Yaakub.

72. (Mkewe Ibrahim) akasema; Ee mimi we! Je, nitazaa na hali mimi ni mkongwe na huyu rnume wangu ni mzee sana hakika hili ni jambo la ajabu.

73. Wakasema: Unastaajabu amri ya Mwenyeezi Mungu? Rehema ya Mwenyeezi Mungu na baraka zake iko juu yenu enyi watu wa nyumba hii. Hakika yeye ndiye Mwenye kusifiwa, Mwenye kutukuzwa.

74. Basi khofu ilipomuondoka Ibrahimu, na imemfikia khabari njema, akaanza kubishana nasi juu ya watu wa Luti.

75. Kwa hakika Ibrahimu alikuwa mpole, Mwenye kumuomba sana Mwenyeezi Mungu, Mwepesi wa kurejea.

76. Ewe Ibrahimu! wacha haya kwa sababu amri ya Mola wako imekwisha fika na hakika hao itawafikia adhabu isiyorudishwa.

77. Na Wajumbe wetu walipomfikia Luti, akawahuzunikia na akawaonea dhiki, na akasema: Hii ni siku ngumu.

78. Na wakamjia kaumu yake mbio mbio, na kabla ya haya walikuwa wakifanya maovu. Akasema: Enyi kaumu yangu! hawa binti zangu, wao wametakasika zaidi kwenu, basi mcheni Mwenyeezi Mungu wala msinifedheheshe mbele ya wageni wangu. Je, miongoni mwenu hakuna mtu muongofu?

79. Wakasema: Bila shaka umekwisha jua sisi hatuna haki juu ya binti zako, na hakika unayajua tunayoyataka.

80. Akasema: Laiti ningelikuwa na nguvu kwenu, au nategemea kwenye nguzo yenye nguvu.

81. (Wajumbe) wakasema: Ewe Luti! Sisi ni wajumbe wa Mola wako, hawatakufikia kwa hiyo ondoka pamoja na watu wako wa nyumbani katika sehemu ya usiku, wala yeyote miongoni mwenu asitazame nyuma isipokuwa mke wako. Hakika yeye utampata msiba utakaowapata hao, hakika miadi yao ni asubuhi, je asubuhi siyo karibu?

82. Basi ilipofika amri yetu, tukaifanya juu yake kuwa chini yake, na tukawapigia mvua ya changarawe za udongo mgumu zipandanazo.

83. Zilizotiwa alama kwa Mola wako, na (adhabu) hii haiko mbali na madhalimu.

84. Na kwa (watu wa) Madyan (tulimpeleka) ndugu yao Shua'ybu, akasema:

Enyi watu wangu! mwabuduni Mwenyeezi Mungu nyinyi hamna mungu ila Yeye tu, msipunguze kipimo wala mizani. Mimi nakuoneni mmo katika hali njema, nami nakukhofieni adhabu ya siku izungukayo.

85. Na enyi watu wangu! timizeni kipimo na mizani kwa uadilifu wala msiwapunguzie watu vitu vyao, wala msieneze uovu katika nchi (mkafanya) uharibifu.

86. (Mali) aliyobakisha Mwenyeezi Mungu ndiyo bora kwa ajili yenu, ikiwa nyinyi ni wenye kuamini, wala mimi si mlinzi wenu.

87. Wakasema: Ewe Shua'yb! Je, swala yako inakuamuru tuyaache waliyokuwa wakiyaabudu baba zetu, au (tuache) kufanya tupendavyo katika mali zetu? Bila shaka wewe ni mpole sana, muongofu.

88. Akasema: Enyl watu wangu! mnaonaje kama ninayo dalili ya wazi itokayo kwa Mola wangu, na ameniruzuku riziki njema kutoka kwake? Wala sipendi kupingana nanyi kwa kufanya yale ninayokukatazeni. Sitaki ila kutengeneza ninavyoweza na sipati kuwezeshwa (haya) ila kwa Mwenyeezi Mungu kwake ninategemea, na kwake naelekea.

89. Na enyi watu wangu! kukhalifiana nami kusije wasababishia nyinyi hata yakakupateni kama yaliyowapata watu wa Nuhu au watu wa Hudi au watu wa Saleh, na watu wa Luti si mbali nanyi.

91. Wakasema: Ewe Shua'yb hatufahamu mengi ya hayo uyasemayo na bila shaka sisi tunakuona mdhalilifu kwetu. Na kama sijamaa zako tungekupiga mawe, wala wewe si mtukufu kwetu.

92. Akasema: Enyi watu wangu! Watu wangu ni watukufu zaidi kwenu kuliko Mwenyeezi Mungu? Na mmemfanya yeye kuwa nyuma ya migongo yenu, Hakika Mola wangu anayazunguka mnayoyatenda,

93. Na Enyi watu wangu! Fanyeni muwezavyo, mimi (pia) ninafanya hivi karibuni mtajua ni nani itakayemfikia adhabu ifedheheshayo na ni nani aliye mwongo. Na ngojeni, mimi (pia) ninangoja pamoja nanyi.

94. Na ilipofika amri yetu, tukamuokoa Shua'yb na wale walioamini pamoja naye kwa rehema yetu, na wale waliodhulumu (adhabu) ukelele ulinyakua (roho zao) na wakawa majumbani mwao wameanguka kifudifudi.

95. Kama kwamba hawakuwamo humo. Sikilizeni! wameangamia watu wa Madyan kama walivyoangamia Thamudi.

96. Na hakika tulimpeleka Musa pamoja na Aya zetu na hoja zilizo wazi.

97. Kwa Firaun na wakuu wake, lakini wao walifuata amri ya Firaun, na amri ya Firaun haikuwa yenye uongofu.

98. Siku ya Kiyama (Firaun) atawatangulia watu wake na atawafikisha Motoni. Na ni pabaya mno mahala hapo panapofikiwa.

99. Na wamefuatishiwa laana katika (dunia) hii na siku ya Kiyama. Ni mbaya mno zawadi watakayopewa.

100. Hizo ni katika khabari za miji tunayokusimulia, baadhi yao ipo na mingine imefutwa.

101. Nasi hatukuwadhulumu, lakini wao wamejidhulumu wenyewe, na waungu wao waliokuwa wakiwaabudu badala ya Mwenyeezi Mungu hawakuwafaa kitu ilipofika amri ya Mola wako, na hawakuwazidishia ila maangamizo.

102. Na hivyo ndivyo kutesa kwa Mola wako kunavyokuwa, anapowatesa (watu wa) miji wakati wakiwa wanadhulumu. Hakika teso lake linaumiza (tena) kali.

103. Kwa hakika katika hayo kuna mazingatio kwa yule anayeogopa adhabu ya Akhera. Hiyo ndiyo siku itakayokusanywa watu, na hiyo ndiyo siku itakayoshuhudiwa.

104. Na hatuiakhirishi ila kwa muda unaohesabiwa.

105. Siku itakapofika, rntu yeyote hatasema ila kwa ruhusa yake, basi baadhi yao watakuwa mashakani na wenye furaha.

106. Na ama wale wa mashakani (wao watatiwa) Motoni, humo watapiga kelele na kutoa kwikwi.

107. Watakaa humo milele muda wa kudumu mbingu na ardhi, isipokuwa apendavyo Mola wako. Hakika Mola wako hufanya apendavyo.

108. Na ama wale waliobahatika, basi watakuwa Peponi, watakaa humo milele muda wa kudumu mbingu na ardhi, isipokuwa apendavyo Mola wako, ni zawadi isiyokwisha.

109. Basi usiwe na shaka juu ya wanayoyaabudu hawa. Hawaabudu ila kama walivyoabudu baba zao zamani, na bila shaka sisi tutawapa sehemu yao kamili bila ya kupunguzwa.

110. Na kwa hakika tulimpa Musa Kitabu, lakini zikatiwa khitilafu ndani yake. Na kama si neno lililotangulia kutoka kwa Mola wako, bila shaka ingelihukumiwa baina yao. Na hakika wao wamo katika shaka inayohangaisha juu yake.

111. Na hakika Mola wako atawapa hao wote malipo ya vitendo vyao kamili kwa sababu yeye anazo khabari za wanayoyatenda.

112. Basi (ewe Mtume) endelea kama ulivyoamuriwa wewe na yule anayeelekea (kwa Mwenyeezi Mungu) pamoja nawe, wala msiruke mipaka. kwani yeye anayaona mnayoyatenda.

113. Wala msiwategemee wale waliodhulumu usije ukakuguseni Moto. Na hamtakuwa na walinzi badala ya Mwenyeezi Mungu, kisha hamtasaidiwa.

114. Na simamisha swala katika sehemu mbili za mchana na nyakati za usiku hakika mema huyaondoa maovu, huo ndio ukumbusho kwa wenye kukumbuka.

115. Na subiri, kwani hakika Mwenyeezi Mungu hapotezi ujira wa wafanyao wema.

116. Basi kwa nini hawakuwamo katika watu wa kabla yenu watu wenye akili, wenye kukataza uharibifu katika nchi isipokuwa wachache tuliowaokoa miongoni mwao. Na wale waliodhulumu walifuata waliyostareheshewa, na wakawa waovu.

117. Na hakuwa Mola wako kuiangamiza miji kwa dhulma na hali watu wake ni wenye kutenda mema.

118. Na kama Mola wako angelipenda bila shaka angeliwafanya watu kuwa umati mmoja, na wataendelea kukhitilafiana.

119. Isipokuwa yule ambaye Mola wako amemrehemu, na kwa (rehema) hiyo amewaumba. Na limetimia neno la Mola wako, lazima nitaijaza Jahannam kwa majinni na watu.

120. Na tunakusimulia katika khabari za Mitume ambazo kwa hizo tunauthibitisha moyo wako. Na katika haya imekufikia haki na mawaidha na ukumbusho kwa wenye kuamini.

121. Na waambie wale wasioamini: Fanyeni muwezavyo, nasi (pia) tunafanya.

122. Na ngojeni, hakika sisi tunangoja.

123. Na ni vya Mwenyeezi Mungu tu vyote vilivyofichikana katika ardhi na mbingu na mambo yote yatarejeshwa kwake. Basi mwabudu Yeye na mtegemee, na Mola wako haghafiliki na yale mnayoyatenda.