Qur'ani Tukufu

Tarjuma ya Qur'ani Tukufu Kwa Kiswahili

Sheikh Ali Muhsin Al-Barwani  (Nani Yeye?)

94. SURAT ASH-SHARH'

(Imeteremka Makka)

Inathibitisha Sura hii kwamba Mwenyezi Mungu ameukunjua moyo wa Nabii wake, na akaufanya ndipo pahala pa kuteremkia siri na ilimu, na akaondoa matatizo yaliyo kuwa yakimthakilisha mgongo wake, nayo ni katika mizigo ya kazi ya Da'wa, yaani Wito. Na akalikutanisha jina lake Mwenyezi Mungu na jina lake Mtume katika asli ya Imani na alama za Dini. Kisha Aya hizi zikataja sunna ya Mwenyezi Mungu ya kuambatisha mepesi na mazito, dhiki na faraji, na zikamtaka Mtume kila anapo pata nafasi kutokana na kutenda kheri, atende kheri nyengine, na afanye lengo lake ni Mola wake Mlezi, kwani Yeye ni Muweza wa kumsaidia.

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU

1. Hatukukunjulia kifua chako? *

2. Na tukakuondolea mzigo wako, *

3. Ulio vunja mgongo wako? *

4. Na tukakunyanyulia utajo wako? *

5. Basi kwa hakika pamoja na uzito upo wepesi, *

6. Hakika pamoja na uzito upo wepesi. *

7. Na ukipata faragha, fanya juhudi. *

8. Na Mola wako Mlezi ndio mshughulikie.  *


Ukitaka kusoma Sura nyengine Rejea uliko toka

Ukiwa una shauri au maelezo juu ya tarjuma hii, andika kwa anwani hii qurani-tukufu@geocities.com

Copyright © 22 August 1997, Sheikh Ali Muhsin Al Barwani