Qur'ani Tukufu

Tarjuma ya Qur'ani Tukufu Kwa Kiswahili

Sheikh Ali Muhsin Al-Barwani (Nani Yeye?)

76. SURAT AL-INSAN

(Imeteremka Madina)

Sura hii imekusanya maneno juu ya kuumbwa kwa binaadamu na kujaribiwa kwake, na kutayarishwa kwake aweze kumshukuru Mwenyezi Mungu au kumkufuru. Na imekusanya mazungumzo juu ya malipo ya makafiri; na imefafanua neema alizo wafadhili Mwenyezi Mungu Waumini, kisha ikageukia kusema na Mtume wa Mwenyezi Mungu s.a.w. na kumtajia alivyo neemeshwa kwa kuteremshiwa Qur'ani, na ikamuamrisha asubiri na adumu katika ut'iifu. Na Sura inawaonya wanao ipenda dunia wakaifadhilisha kuliko Akhera, na ikasimulia kwa mawaidha ya Aya hizi, na ikakhusisha kunafiika kwazo pindi akipenda Mwenyezi Mungu Mtukufu, na ikazifanya rehema za Mwenyezi Mungu na adhabu zake kuwa zinategemea hukumu yake na pendo lake.

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU

1. Hakika kilimpitia binaadamu kipindi katika zama ambacho kwamba hakuwa kitu kinacho tajwa. *

2. Hakika Sisi tumemuumba mtu kutokana na mbegu ya uhai iliyo changanyika, tumfanyie mtihani. Kwa hivyo tukamfanya mwenye kusikia, mwenye kuona. *

3. Hakika Sisi tumembainishia Njia. Ama ni mwenye kushukuru, au mwenye kukufuru. *

4. Hakika Sisi tumewaandalia makafiri minyororo na pingu na Moto mkali. *

5. Hakika watu wema watakunywa katika vinywaji vilivyo changanyika na kafuri, *

6. Ni chemchem watakao inywa waja wa Mwenyezi Mungu, wakiifanya imiminike kwa wingi. *

7. Wanatimiza ahadi, na wanaiogopa siku ambayo shari yake inaenea sana, *

8. Na huwalisha chakula, juu ya kukipenda kwake, masikini, na yatima, na wafungwa. *

9. Hakika sisi tunakulisheni kwa wajihi wa Mwenyezi Mungu. Hatutaki kwenu malipo wala shukrani. *

10. Hakika sisi tunaiogopa kwa Mola wetu Mlezi hiyo siku yenye shida na taabu. *

11. Basi Mwenyezi Mungu atawalinda na shari ya siku hiyo, na atawakutanisha na raha na furaha. *

12. Na atawajazi Bustani za Peponi na maguo ya hariri kwa vile walivyo subiri. *

13. Humo wataegemea juu ya viti vya enzi, hawataona humo jua kali wala baridi kali. *

14. Na vivuli vyake vitakuwa karibu yao, na mashada ya matunda yataning'inia mpaka chini. *

15. Na watapitishiwa vyombo vya fedha na vikombe vya vigae, *

16. Vya fedha safi kama kiyoo, wamevipima kwa vipimo. *

17. Na humo watanyweshwa kinywaji kilicho changanyika na tangawizi. *

18. Hiyo ni chemchem iliyo humo inaitwa Salsabil. *

19. Na watawazungukia kuwatumikia wavulana wasio pevuka, ukiwaona utawafikiri ni lulu zilizo tawanywa. *

20. Na utakapo yaona, utakuwa umeona neema na ufalme mkubwa. *

21. Juu yao zipo nguo za hariri laini za kijani kibichi, na hariri nzito ya at'ilasi. Na watavikwa vikuku vya fedha, na Mola wao Mlezi atawanywesha kinywaji safi kabisa. *

22. Hakika haya ni malipo yenu; na juhudi zenu zimekubaliwa. *

23. Hakika Sisi tumekuteremshia Qur'ani kidogo kidogo. *

24. Basi ngojea hukumu ya Mola wako Mlezi wala usimt'ii miongoni mwao mwenye dhambi au mwenye kufuru. *

25. Na likumbuke jina la Mola wako Mlezi asubuhi na jioni; *

26. Na usiku msujudie Yeye, na umtakase usiku, wakati mrefu. *

27. Kwa hakika watu hawa wanapenda maisha ya kidunia, na wanaiacha nyuma yao siku nzito. *

28. Sisi tumewaumba, na tukavitia nguvu viungo vyao. Na tukitaka tutawabadilisha mfano wao wawe badala yao. *

29. Hakika haya ni mawaidha; basi anaye taka atashika Njia ya kwenda kwa Mola wake Mlezi. *

30. Wala hamwezi kutaka ila atakapo Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye ilimu, Mwenye hikima. *

31. Humuingiza amtakaye katika rehema yake. Na wenye kudhulumu amewawekea adhabu iliyo chungu.  *  


Ukitaka kusoma Sura nyengine Rejea uliko toka

Ukiwa una shauri au maelezo juu ya tarjuma hii, andika kwa anwani hii qurani-tukufu@geocities.com

Copyright © 22 August 1997, Sheikh Ali Muhsin Al Barwani